Klabu ya Simba SC imetozwa faini ya jumla ya shilingi milioni 10 kufuatia makosa mawili ya kinidhamu yaliyotokea katika mchezo wa Dabi ya Kariakoo dhidi ya Young Africans SC. Mchezo huo ulipigwa mwezi Machi katika Uwanja wa New Amaan Complex na kumalizika kwa sare ya bila kufungana.

Bila kusahau meridianbet ndio wakali wa ODDS KUBWA, Machaguo zaidi ya 1000 na kila kitu ukitakacho. Bashiri kijanja hapa
Kwa mujibu wa taarifa za ma mlaka za soka, Simba imetozwa faini ya shilingi milioni tano baada ya timu hiyo kuingia uwanjani kupitia mlango usio rasmi badala ya ule uliotengwa kwa ajili ya timu zinazoshiriki mchezo.

Adhabu nyingine ya shilingi milioni tano imetolewa baada ya klabu hiyo kukataa kutumia chumba rasmi cha kuvalia kilichotengwa kwa ajili ya timu yao katika uwanja huo. Hatua hiyo imeelezwa kuwa ni kinyume na taratibu na kanuni za uendeshaji wa mechi za ligi.

Mbali na faini hizo, Simba pia imeagizwa kulipia gharama za matengenezo ya mlango wa chumba cha mkutano wa wanahabari uliodaiwa kuharibika wakati wa tukio hilo, ikiwa ni sehemu ya kuwajibika kwa uharibifu uliotokea katika eneo la uwanja.

Katika hatua nyingine za kinidhamu, mshambuliaji wa Simba, Selemani Mwalimu, amefungiwa michezo mitatu na kutozwa faini ya shilingi milioni moja baada ya kupatikana na hatia ya kumpiga kwa kutumia kiwiko mchezaji wa Dodoma Jiji FC, Andy Bikoko, katika mchezo wa ligi.

Kutokana na adhabu hiyo, Selemani Mwalimu atakosa michezo mitatu ijayo ambayo ni dhidi ya B19 FC katika mashindano ya CRDB Bank Federation Cup pamoja na michezo ya Ligi Kuu dhidi ya Singida Black Stars na Tanzania Prisons.

Wakati huohuo, beki wa Simba, David Kameta, ametozwa faini ya shilingi milioni moja baada ya kuonekana akimwaga kimiminika kiwanjani wakati timu hiyo ilipofanya ziara ya uwanjani dakika chache baada ya kuwasili katika Uwanja wa Amaan. Kitendo hicho kilitafsiriwa kuwa na viashiria vya imani za kishirikina na adhabu hiyo imetolewa kwa mujibu wa Kanuni ya 41:5(5.5) ya Ligi Kuu inayohusu udhibiti wa wachezaji.


