KOCHA Mkuu wa Ihefu, Juma Mwambusi katika kipindi hiki cha mapumziko amewajenga wachezaji wake kisaikolojia kuelekea michezo ijayo ya ligi.
Mwambusi amechukua mikoba ya kukinoa kikosi hicho hivi karibuni ambapo alisimamia mechi moja ya ligi dhidi ya KMC ambayo walipoteza kwa mabao 2-1.
Akizungumzia maandalizi yao, Mwambusi amesema kuwa “Tunamshukuru Mungu kikosi kinaendelea na maandalizi kuelekea mchezo wetu unaofuata wa ligi dhidi ya Tanzania Prisons.
“Unajua timu inapofungwa mechi zaidi ya moja wachezaji wanaharibika saikolojia zao hivyo nimeanza na hilo kwenye mazoezi yangu ili kurudisha morali katika timu kwa ajili ya kuhakikisha tunapata ushindi katika mchezo ujao.”
Timu ya Ihefu inatarajia kucheza mechi yao ya ligi inayofuata dhidi ya Tanzania Prisons Oktoba 4 mwaka huu kwenye Uwanja wa Highland Estates, Mbarali mkoani Mbeya.