Kuelekea msimu ujao, Man United ipo kwenye mchakato wa kufanya usafi wa kikosi chao. Wapo watakaoondoka mazima, wapo wa mkopo na wapo wapya watakaoingia.
Jadon Sancho yupo mbioni kujiunga na United baada ya mchakato wa kumsajili kubuma tangu wakati wa Jose Mourinho. Kwa hatua ilipofikia sasa, ni suala la muda tu kabla ya Sancho kutangazwa rasmi kama mchezaji wa United.
Ujio wa Sancho ni changamoto kubwa kwa Anthony Martial, mshambuliaji huyu ambaye amekuwa nje ya uwanja tangu mwezi Machi atakuwa na kibarua cha ziada kupambania namba kwenye kikosi cha kwanza.
Martial atapambana na Sancho, Rashford, Greenwood, Cavani, James na Mata kitu ambacho kiuhalisia ni changamoto kwake na hivyo kunauwezekano mkubwa akawekwa sokoni punde Sancho atakapotua United.

Sambamba na Martial, Donny Van De Beek amekuwa na msimu mgumu ndani ya Man United baada ya kujiunga na klabu hiyo akitokea Ajax msimu uliopita. Japokuwa Van De Beek mwenyewe anataka kubaki United na kupambania nafasi yake, klabu hiyo ipo wazi kupokea dau lenye uhalisia ili kumuachia mchezaji huyo kwa timu inayomtaka.
Jesse Lingard, Andreas Pereira, Diogo Dalot na Axel Tuanzebe ni miongoni mwa wachezaji wanaoweza kutolewa kwa mkopo kwa mara nyingine kama sio kuuzwa moja kwa moja. Hii ni kutokana na uhalisia kuwa wachezaji hawa hawana namba za kudumu kwenye kikosi cha Ole Gunnar Solskjaer.

Vijana, Anthony Elanga, Amad Diallo, Shola Shoretire na Hannibal Mejbri bado haijajulikana kama watatolewa kwa mkopo au watabakizwa kikosini hapo kama sehemu ya kuwaendeleza wakati huu ambao wamejuimishwa kwenye kikosi cha wakubwa.
Pamoja na Sancho, Man United inahusishwa na usajili wa Rafael Varane, Pau Torres, Kieran Trippier ikiwa ni pamoja na mikataba mipya kwa Paul Pogba na Juan Mata huku hatma ya David De Gea ikiwa haijajulikana kuelekea msimu ujao.


