Kocha Mkuu wa Yanga SC, Pedro Goncalves, amesema kikosi chake kinatarajia mchezo mgumu dhidi ya Mbeya City utakaochezwa Aprili 16, 2026, katika muendelezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara. Goncalves ameeleza kuwa wapinzani wao wako katika kiwango kizuri kwa sasa, jambo linaloongeza ushindani katika mchezo huo muhimu.

“Tunategemea mchezo mgumu kesho, mgumu kwa kiwango kikubwa kutokana na ubora wa wapinzani wetu kwa sasa,” amesema Goncalves.
Bila kusahau meridianbet ndio wakali wa ODDS KUBWA, Machaguo zaidi ya 1000 na kila kitu ukitakacho. Bashiri kijanja hapa
Licha ya ugumu huo, kocha huyo ameweka wazi kuwa kikosi chake kimefanya maandalizi ya kutosha kuhakikisha wanapata matokeo chanya. Ameongeza kuwa malengo yao makuu ni kuondoka na alama tatu ili kuendelea kujiweka katika nafasi nzuri ya ubingwa msimu huu. “Tumejiandaa vizuri na lengo letu kubwa ni kupata alama tatu,” ameongeza Goncalves.
Kwa upande wa mchezaji wa Yanga, Israel Mwenda, amekiri kuwa mchezo huo hautakuwa rahisi lakini wamejipanga kupambana hadi mwisho ili kuepuka kupoteza mwelekeo katika mbio za ubingwa. “Tunajua utakuwa mchezo mgumu lakini tutajituma zaidi ili kupata matokeo na kubaki kwenye mbio za ubingwa,” amesema Mwenda.
Kwa upande wa Mbeya City, Kocha Mkuu Mecky Maxime amesema wanatambua ukubwa wa mchezo huo na presha iliyopo, hasa kutokana na nafasi za timu hizo kwenye msimamo wa ligi. Hata hivyo, ameahidi kuwa wataingia uwanjani kwa tahadhari na heshima kwa wapinzani wao.“Italeta presha sana kutokana na matokeo yetu na sehemu tuliyopo, lakini tutacheza kwa umakini na kumheshimu mpinzani wetu,” amesema Maxime.
Naye mchezaji wa Mbeya City, Abdi Abdallah, ameongeza kuwa watafuata maelekezo ya benchi la ufundi na kupambana kwa nguvu zote ili kuonesha kiwango walichokionyesha katika maandalizi yao ya hivi karibuni, wakiamini wana uwezo wa kufanya vizuri kwenye mchezo huo.

