KLABU ya KMC baada ya kutangaza kuingia udhamini mpya bila kutaja ni kiasi gani watapata kwenye udhamini huo hatimaye sasa mambo yamewekwa hadharani na mwenyekiti wa klabu hiyo Songolo Mjanja kuwa dili hilo ni la kiasi cha Tsh 300M.
Klabu hiyo imefanikiwa kuingia makubaliano na kampuni ya kubashiri michezo ya Meridian Bet wa miaka mitatu wenye thamani ya zaidi ya milioni 300, ambayo ni karibu mara tatu zaidi ya mkataba wa awali.
Klabu hiyo ilisaini makubaliano hayo kwenye ofisi za KMC zilizopo Magomeni jijini Dar, huku mwenyekiti wa klabu hiyo Songolo Mjanja akijinasibu kuwa mpunga ambao watavuna ni mara mbili ya ule ambao walikuwa wanavuna kwa mdhamini aliyepita.
“Tumeingia makubaliano ya udhamini wa klabu yetu na Meridian Bet, ambao watakaa mbele kwenye jezi zetu. Huu ni udhamini wa miaka mitatu ambao tutavuna kila mwaka zaidi ya milioni 100.
“Ni fedha nyingi ambayo ni mara tatu zaidi ya ile ambayo tulikuwa tunapata awali na kampuni nyingine. Meridian watakaa mbele kwenye jezi yetu kwa miaka mitatu,” alisema.