Uwanja wa Aviva mjini Dublin unaripotiwa kuwekwa katika hali ya kusubiri kuandaa mechi za mashindano ya Ulaya kwa vilabu vya Uingereza wiki ijayo.
Ratiba ya wikiendi hii ya mechi za Ligi Kuu ya Uingereza pamoja na mechi za EFL, zote zimeahirishwa kufuatia kifo cha Malkia Elizabeth II, huku nchi ikitumikia siku kumi za maombolezo ya kitaifa.

Tahadhari sasa itageukia hatima ya mechi za Ulaya katikati ya wiki. Klabu za Liverpool, Tottenham, Chelsea na Manchester City zote zitacheza Ligi ya Mabingwa wiki ijayo, huku Arsenal na Man United zikicheza Europa League na West Ham kwenye Europa Conference League.

Vilabu vya Ligi ya Uingereza vinafikiriwa kuwa na hamu ya kutimiza mechi katika mashindano ya UEFA ili kuepusha mrundikano wa mechi, hata kama itatokeaa kuwahamishia kwenye uwanja usio na upande wowote “neutral ground“, huku ikitazamiwa kuwa uwanja wa Aviva-Dublin ndio utakaotumika kwa timu za Uingereza ambazo wanakabiliwa na msiba wa kitaifa.

Ratiba ya wiki ijayo itawakutanisha Liverpool wakiwakaribisha Ajax kwenye Uwanja wa Anfield siku ya Jumanne, huku Rangers wakiwa nyumbani kumenyana na Napoli usiku huo huo katika michezo yao ya Makundi ya Ligi ya Mabingwa.
Jumatano, Chelsea watakuwa uwanjani kucheza na Red Bull Salzburg kwenye Uwanja wa Stamford Bridge, na Manchester City wakiwakaribisha Borussia Dortmund kwenye Uwanja wa Etihad.

Wakati Alhamisi usiku Arsenal watakuwa nyumbani katika mechi ya Ligi ya Europa, watakapocheza na PSV Eindhoven kwenye Uwanja wa Emirates.
Bado kuna uwezekano wa Rangers kuhamisha mchezo wao hadi uwanja wa Aviva na Finn Park chaguo jingine linalowezekana, lakini mji mkuu wa Ireland unasalia kuwa kipenzi cha vilabu vya Kiingereza kwa ukaribu wake rahisi.

