Azam Kutimkia Misri

UONGOZI wa kikosi cha Azam umethibitisha rasmi kuwa leo Ijumaa unatarajia kuondoka nchini kwenda Misri kwa ajili ya kambi yao ya kabla ya msimu ‘Preseason’ ambayo itakuwa katika jiji la El Gouna.

Kambi hiyo ya Misri inatarajiwa kuwa sehemu ya pili ya kambi ya Azam ambao walianza sehemu ya kwanza ya kambi yao katika Uwanja wa Azam Complex Julai 18, mwaka huu ambapo kambi hiyo inahusisha wachezaji wote wa kikosi hicho wakiwemo wachezaji wao saba ambao wamesajiliwa katika dirisha la usajili.

Azam inakuwa timu ya pili kutoka Tanzania kwenda nchini Misri mara baada ya Simba ambao walianza kambi yao huko Misri Alhamisi ya Julai 14, mwaka huu.

Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Azam, Zakaria Thabith ‘Zaka Zakazi’ alisema: “Timu yetu leo Alhamisi inatarajia kumaliza sehemu ya kwanza ya Kambi yetu ya kabla ya msimu hapa Dar es Salaam, ambapo kesho (leo), Ijumaa tunatarajia kusafriri kwenda nchini Misri kwa ajili ya sehemu ya pili ya maandalizi ya msimu mpya.

“Kama ambavyo tuliweka wazi hapo awali tunatarajia kuweka kambi katika jiji la El Gouna ambako kuna mahitaji yote ya kuifanya timu yetu kuwa bora kwa ajili ya mashindano ya ndani na yale ya kimataifa.”

Acha ujumbe