Beki wa kati wa Simba raia wa Kenya Joash Onyango amekiri kuwa ni kweli aliandika barua ya kutaka kuondoka kwenye klabu hiyo baada ya kutoridhishwa na baadhi ya mambo ambayo hakuwa tayari kuyataja kwa wakati huo.
Oyango alisema kuwa kwa sasa mpango huo haupo tena kwa sababu amesharejea kwenye timu na kila kitu kipo sawa na wanasimba wote wajue kuwa yeye ni mchezaji wa Simba na atakuwa miongoni mwa wachezaji ambao wataipambania timu hiyo msimu huu.
Akizungumza juzi akiwa jijini Mbeya baada ya mchezo wa Prisons na Simba wakishinda bao 1-0 Onyango alisema: “Ni kweli niliandika barua ya kuomba klabuni hapo. Lakini nashukuru viongozi wangu walinisikiliza nilichokuwa nahitaji na sasa nimerejea tena.
“Kwa maana hiyo mashabiki watambue kuwa mimi ni mchezaji wao na nitakuwepo hapa kwa msimu mzima kuendelea kuipambania timu yangu.”
Onyango alicheza mchezo wake wa kwanza msimu huu juzi Jumatano, baada ya kuingia kipindi cha pili kwenye mchezo wa ligi dhidi ya Tanzania Prisons akichukua nafasi ya Henock Inonga Backa.