NABI: Wahenga walisema ‘lisemwalo lipo’, kama bado basi laja! huu ni msemo maarufu sana kwa mtu akitaka kujihakikishia jambo kuwa litatokea muda wowote kuanzia wakati huo.
Hivyo ndivyo unavyoweza kusema kwa Kocha mkuu wa klabu ya Yanga Nasraddine Nabi, Taarifa za ndani kutoka klabuni hapo zinasema kuwa tayari kocha huyo ameshamalizana na mabosi na kilichosalia ni kutangazwa tu kwa taarifa rasmi ya klabu kuhusu kuachana na kocha huyo.
Sababu inayodhaniwa kuwa imepelekea uongozi wa klabu ya Yanga kufikiria kumtimua Nabi, ni mwenendo mbovu wa matokeo ndani ya uwanja, hususani kwenye upande wa michezo ya kimataifa, kwani matumaini ya Yanga yalikuwa ni kufuzu hatua ya makundi Ligi ya Mabingwa barani Afrika, lakini kwa bahati mbaya wameondolewa na AL Hilal ya Sudan.
Katika michezo ya kimataifa ambayo Yanga ya Nabi amecheza msimu huu, Kacheza michezo 4 ya CAFCL, ameshinda 2 dhidi ya Zalan FC, sare 1 na amepoteza mchezo mmoja dhidi ya AL Hilal.
Nasraddine Nabi aliwasili Yanga mwaka jana tarehe 21, Aprili 2021, na kufanikiwa kutwaa ubingwa wa Ligi, FA na Ngao ya Jamii mara 2, huku akiweka rekodi nzuri ya kutokufungwa kwenye Ligi mpaka sasa akiwa amecheza jumla ya michezo 43 kwa mujibu wa Afisa Habari wa Klabu hiyo Ali Kamwe “Yanga ina mechi ya 43 leo haijapoteza mchezo” Alisema Kamwe.