Safari nzima ilitamatikaka pale Keko ya Dar es Salaam tarehe 17 Mei 2012. Nani haikumbuki taharuki ya asubuhi ile? Ilikuwa habari kila kona ya mtaa. Tumempoteza fundi mjenzi na fundi mkarabati wa mpira, Patrick Mutesa Mafisango.
Nani haukumbuki mwili wake unaovuja jasho baada ya dakika ya pili tu ya mchezo? Nani haikumbuki miguu yake iliyokanyaga kila jani la uwanja kuusaka mpira? Pale kati kwenye dimba la chini, angetokea na sura na Claudie Makelele wakati mnafukuza mpira, alafu ghafla unaiona miguu ya Fabregas mkishaupata. Mkifika eneo mwisho mnamuona Zinedine Zidane aliyeota nywele. Alijitafsiri vema kama box-box midfielder.

Akiwa katikati ya kizungumkuti sawa na Miroslav Klose na Eduardo Da Silva, yeye aliifuata falsafa ya Simeone Perotta. Alichagua kulitumikia taifa la Rwanda, licha ya kuwa mzaliwa wa Kinsasha na raia halali wa Jamuhuri ya Kidemokrasia ya watu wa Congo.
Kwani nani ameusahau ubingwa wa Simba 2012? Juu yake yupo mnyamwezi Haruna Moshi na rasta zake, pembeni yake afande Mwinyi Kazimoto anapiga patrol, kwenye mashavu ana Emanuel Okwi na Uhuru Suleiman wanawafanyisha mafull back mazoezi ya olympic. Yeye alikuwa kama mwalimu wa zamu. Anahakikisha wote wapo. Alikuwa anawalisha mipira kama mgonjwa wa ICU. Licha ya kucheza kiungo wa kukaba, hadi anafariki alikuwa kinara wa mabao. Alishachana nyavu mara 12.
Kaka Mafisango..Ile siku unaipigania Simba mpaka tone la mwisho la damu yako pale Sudan dhidi ya Al Ahyl Shandy, kumbe ndio mechi yako ya mwisho. Unatuaga kwa kukosa tuta. Hatukukuzoea hivo. Ukaamua utuage kwa tofauti ya tulivokuzoea. Kama ulituonea aibu ungemshtua hata mshikaji wako Okwi atuambie.
Ndugu zako Rwanda wanakulilia, hawaamini umecheza mechi 23 tu. Mdogo wako Haruna Niyonzima bado anakulilia, anasema hajakuonesha uliyomfunza pale APR.
Laiti kama funguo za mauti zingemilikiwa na binadamu, basi tungefanya juu chini urudi, tukuone walau kwa mara moja ya mwisho. Wote tunajua kazi ya Mungu haina makosa, ila tunabaki kuwa binadamu. Mioyo yetu ni migumu sana kuupokea ukweli. Bado tunakulilia. Walau tukuoneshe tunavokuthamini.


Zeiyana
Daaah..! Mafisango alikua mchezaji mwenye mbinu yingi sana hadi leo hajatokea mbadala yake..! r i p