Soka la Ghana limeingia katika maombolezo kufuatia kifo cha mchezaji chipukizi Dominic Frimpong, aliyekuwa akiichezea kwa mkopo Berekum Chelsea kutoka Aduana FC, baada ya kupigwa risasi na majambazi waliovamia basi la timu hiyo.
Tukio hilo la kusikitisha lilitokea usiku wa kuamkia leo Jumatatu wakati kikosi cha Berekum Chelsea kilipokuwa kinarejea kutoka Samreboi kilikocheza mechi ya Ghana Premier League dhidi ya Samartex, ambapo majambazi waliwazuia njiani na kuanza kufyatua risasi.
Bila kusahau meridianbet ndio wakali wa ODDS KUBWA, Machaguo zaidi ya 1000 na kila kitu ukitakacho. Bashiri kijanja hapa
Kwa mujibu wa taarifa ya klabu hiyo, shambulio hilo lilifanyika eneo la Ayiresu kwenye barabara ya Gorso, ambapo watu waliokuwa na silaha walilizingira basi hilo na kuwashambulia wachezaji pamoja na benchi la ufundi.
Klabu hiyo ilielezea tukio hilo kwa huzuni kubwa, ikisema “Tulipokuwa tukirejea Berekum kutoka Samreboi, basi letu lilishambuliwa na majambazi waliokuwa wameziba barabara. Walifyatua risasi huku dereva akijaribu kurudi nyuma, na wachezaji pamoja na viongozi walikimbilia porini kujinusuru,” ilisema taarifa hiyo.
Frimpong mwenye umri wa miaka 20 alipigwa risasi katika shambulio hilo na kupoteza maisha papo hapo, akiacha nyuma ndoto kubwa ya soka iliyokuwa inaanza kung’ara, baada ya kucheza mechi 11 na kufunga mabao mawili msimu huu.
Shirikisho la Soka Ghana, limelaani tukio hilo na kutoa salamu za pole, likisema “Hili ni pigo kubwa si tu kwa Berekum Chelsea bali kwa soka la Ghana kwa ujumla. Frimpong alikuwa kipaji chipukizi chenye matumaini makubwa,” huku Jeshi la Polisi Ghana likithibitisha kuanza msako mkali kuwatafuta wahusika wa tukio hilo.

