Azam: Tepsie Kuongeza Nguvu Stars

Mchezaji nyota kinda wa klabu ya Azam FC Tepsie Evance ameongezwa kwenye kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kinachojiandaa na mchezo wa kufuzu fainali za CHAN dhidi ya Uganda ‘The Cranes’.

Kikosi cha Taifa Stars kinachonolewa na Kocha Mkuu, Kim Poulsen kimeanza mazoezi ya kujiandaa na mchezo huo utakaopigwa Agosti 28, siku ja jumapili kwenye uwanja wa Benjamini Mkapa Dar es salaam.

Awali waliitwa nyota 25 kwenye kikosi hicho, lakini jina la Tepsie halikuwemo katika kikosi hicho licha ya kufanya vyema kwenye ligi kuu ya Tanzania akiwa na kikosi cha Azam.

Lakini kwa sasa Tepsie amejumuishwa kwenye kikosi hicho akiwa kama mbadala wa Abdul Seleman ambaye ameondolewa kikosini kwa sababu anasumbuliwa na majeraha.

Akizungumzia hali ya kambi, Meneja wa Stars, Nadir Cannavaro amesema kuwa: “Morali ya wachezaji ni kubwa na kila mmoja anahitaji kuwa sehemu ya mchezo dhidi ya Uganda ili kutimiza malengo ya timu na malengo binafsi.”

Acha ujumbe