BAADA ya kumaliza ligi katika nafasi ya nane kwenye msimamo, Uongozi wa Polisi Tanzania kwa sasa umeweka mikakati ya kuwasajili nyota wa kimataifa kwa ajili ya kuboresha zaidi kikosi chao kwa msimu ujao.
Polisi Tanzania ambayo inanolewa na Kocha Mkuu, Malale Hamsin wamekuwa na sheria ya kusajili wachezaji wazawa katika kikosi tangu kuanzishwa kwa timu hiyo.

Akizungumzia mikakati yao katika dirisha kubwa la usajili ambalo limefunguliwa Julai mosi mwaka huu, Ofisa Habari wa Polisi Tanzania, Hassan Juma amesema kuwa kwa sasa watafanya maboresho ya sheria hiyo.
“Tutafanya maboresho zaidi kwenye kikosi chetu ili kuhakikisha malengo yetu ya msimu ujao ambayo tutayaweka yanatimia.
“Tumepanga kufanya maboresho ya sheria yetu ya kusajili wachezaji wazawa tu na badala yake kwa msimu ujao tutakuwa na wachezaji wa kimataifa kwa asilimia chache.”